
Lolote mfanyalo, lifanyeni kwa moyo, kama kwa Bwana, wala si kwa wanadamu. WAKOLOSAI 3:23
Hatukuumbwa kuishi maisha ya kuchosha. Mungu aliweka hamu ya vituko ndani yetu, na vituko vinamaanisha kujaribu kufanya kitu ambacho hajawahi kufanya. Iwapo utakuwa mwenye vituko, huenda ukahitaji kutoka nje kufanya jambo jipya. Usikae kando katika maisha ukitazama watu wajasiri wakiishi maisha ya kusisimua—jiunge nao. Toka katika “jahazi lako la usalama” na uone kama unaweza kutembea juu ya maji vile Petro alivyofanya (tazama Mathayo 14:26–31).
Ninakuhakikishia kwamba iwapo utatoka nje hadi kwenye mapenzi ya Mungu juu yako, atafanya uweze kufanikiwa. Huhitaji kuhisi kuwa unaweza, na si lazima uwe na tajriba. Kile unachohitaji ni hamu ya kuwa mtiifu kwa Mungu, moyo wenye shukrani, na moyo uliojaa imani. Mungu hatafuti uwezo; anatafuta kupatikana. Anatafuta atakayesema, “Niko hapa, Mungu, nitume. Niko hapa, nitumie. Ninataka kukutumikia, Mungu. Ninataka kufanya yote unayotaka nifanye.”
Sala ya Shukrani
Baba, ninashukuru kwamba unataka nifurahie maisha ya kushangaza yaliyojaa vituko. Chochote unachotaka nifanye, ninaomba kwamba ukiweke bayana. Asante kwa nafasi unazonitumia na ujasiri unaonipa wa kuzitumia vilivyo.