Sisimka!

Nalifurahi waliponiambia na twende nyumbani kwa Bwana! (Zaburi 122:1)

Kama Wakristo, tuna baraka nyingi sana! Tunaweza kujua Mungu, kusikia sauti yake, kupokea upendo wake, kumtumaini kutufanyia yaliyo mazuri, na kutulia katika ukweli kwamba ana kila kipengele cha maisha yetu chini ya udhibiti wake. Tuna sababu nyingi za kusisimka! Tunasisimka kuhusu vitu aina nyingi, kwa hivyo kwa nini tusiwe wenye kusisimka kuhusu uhusiano wetu na Mungu?

Mara nyingi watu husema kuonyesha msisimko wowote katika muktadha wa kiroho ni “hisia.” Mwishowe, nilitambua kwamba ni Mungu aliyetupatia hisia na kwamba ingawa asingependa tuziruhusu kuongoza maisha yetu, hutupatia kwa kusudi, ambayo ni sehemu ya kufurahia. Iwapo kweli tunamfurahia Mungu, kwa nini tusiweze kuonyesha hisia za upendo huo?  Kwa nini tajriba yetu ya kiroho iwe kavu na yenye kuchusha, isiyochangamsha na isiyo na uhai? Kwani Ukristo unafaa kuonyeshwa kwa sura ndefu, muziki wa huzuni, na kaida za giza? Bila shaka!

Katika andiko la leo, Daudi alisema alifurahia kwenda kwa nyumba ya Mungu. Katika 2 Samweli 6:14, alicheza mbele za Bwana “kwa nguvu zake zote.” Alicheza pia kinubi, akaimbia Mungu, na kufurahia sana. Lakini Daudi aliishi chini ya Agano la Kale. Leo tunaishi chini ya Agano Jipya, sisi ambao tunamwamini Kristo tumejawa tumaini, furaha, na amani (soma Warumi 15:13). Hatuna haja tena ya kung’ang’ana au kutia bidii sana kukubalika na Mungu, lakini tunatulia katika neema ambamo Yesu ametufanya tukubalike. Hatuna haja ya kujaribu kujifanya wenye haki kwa matendo yetu, lakini tumefanywa wenye haki  kwa imani. Tunaweza kusikia sauti yake na kufurahia uwepo wake. Tumewekwa huru kutokana na kila aina ya utumwa! Hizi ni sababu kubwa za kutusisimua!

NENO LA MUNGU KWAKO LEO:

Andika sababu kumi za kukusisimsha kuhusu uhusiano wako na Mungu.  

Facebook icon Twitter icon Instagram icon Pinterest icon Google+ icon YouTube icon LinkedIn icon Contact icon